ad

ad

FAINALI ZA MASHINDANO YA POOL ZAFUNGULIWA RASMI.

 Katiba Tawala wa Wilaya ya Moshi mjini,Remida Ibrahim(wa pili kulia) akicheza kuashilia uzinduzi wa fainali za mashindano ya Pool Taifa yajulikanayo kama “Safari National Pool Competition 2014” yanayofanyika katika Ukumbi wa Kuringe Mkoani Kilimanjaro.Kutoka kushoto ni Katibu wa chama cha Pool Taifa(TAPA), Amos Kafwinga,Meneja wa Bia ya Safari Lager, Oscar Shelukindo na Makamu Mwenyekiti wa TAPA, Fred Mushi.
 Baadhi ya Wachezaji wa Pool wakiwa na zawadi mbalimbali wakielekea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kilimanjaro ya Mawenzi kutoa kwa wagonjwa ikiwa ni sehemu ya kurudisha kwa jamii kile wanachofadhiliwa wa Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) wakati wa ufungunguzi wa mashindano ya Pool Kitaifa yanayofanyika Mkoani humo yajulikanayo kama “Safari National Pool Competition 2014”.
 Baadhi ya wachezaji wa Pool wakitoa zawadi za vitu mbalimbali kwa wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kilimanjaro ya Mawenzi ikiwa ni sehemu ya kurudisha kwa jamii kile wanachofadhiliwa wa Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) wakati wa ufungunguzi wa mashindano ya Pool Kitaifa yanayofanyika Mkoani humo yajulikanayo kama “Safari National Pool Competition 2014”.
WACHEZAJI wa mchezo wa pool nchini wametakiwa kutumia mchezo huo kama sehemu ya ajira kwao  na pia sehemu ya kukukutana na kupeana  mawazo ya kuinuana kimaisha.
Hayo yalisemwa mjini hapa jana na  Katibu Tawala wa Wilaya ya Moshi Mjini,Remida Ibrahim wakati wa ufunguzi rasmi wa  fainali za taifa za mashindano ya ‘Safari Lager National Pool Championship 2014’, zinazofanyika kwenye ukumbi wa Kuringe ambapo yeye alikuwa mgeni rasmi akimwakilisha Mkuu wa wilaya hiyo, Ibrahim Msengi.
Bw. Ibrahim amesema mchezo huo kwa sasa ni ajira kwa wanaoucheza, hivyo ni vema wachezaji wakautumia vizuri kwa ajili ya kuwainua kimaisha badala ya kuutumia kwa masuala ambayo hayana faida katika maisha yao.
“Nitumie nafasi hii kukushukuruni wadhamini wa mchezo huu  kwa kupitia bia ya Safari lager kutokana na kwamba umeongeza ajira kwa vijana, hivyo wachezaji niwasihi tumieni mchezo wa pool kuweza kuinua maisha yenu na pia mnapokutana katika mashindano kama hayo tumieni nafasi hii kushauriana masuala ya msingi ya kuwainua kimaisha,”alisema Ibrahim.
Anasema kazi kubwa iliyofanywa na wadhamini wa mchezo huo ni kubwa ambayo inatakiwa kuigwa na makampuni mengine katika kuinua michezo nchini na pia kuibua ajira kwa vijana.
Ibrahim anasema endapo wachezaji watautumia kama ilivyo lengo la mdhamini la kuuinua na kuupandisha chati kuna uwezekano mkubwa ukailetea sifa Tanzania katika mashindano ya Afrika.
Alisema mwaka jana  timu ya taifa iliweza kuthubuti katika mashindano ya Afrika kwa kushika nafasi ya tatu huku mchezaji Patrick Nyangusi akiibuka bingwa wa Afrika kwa upande wa mchezaji mmoja mmoja (wanaume).
“Kwa kweli niwapongeze kwa kazi hiyo kubwa ya kutuwakilisha vizuri katika mashindano hayo na nina imani mkiendelea hivi kuna uwezekano mkubwa mkatutoa kimasomaso kwa kuchukua ubingwa wa Afrika, hivyo wachezaji ni kazi kubwa kuzidisha nidhamu na mazezi maana bila ya nidhamu hakuna mafanikio yayoweza kupatikana,”akasema.
Naye menaja wa bia ya Safari Lager, Oscar Shelukindo  wakati akizungumza kwenye ufunguzi huo aliwataka wachezaji wa timu zote zinazoshiriki fainali hizo kucheza kwa utulivu hadi mwisho wa fainali hizo.
Shelukindo alisema haitakuwa jambola busara  endapo fainali hizo zitamalizika huku wakiacha gumzo la vitendo  ambazo si vya kiungwana.
“Kwanza niwape pole kwa uchovu wa safari ndefu mlikotoka kwenye mikoa yenu kwa ajili ya kufika hapa kushiriki fainali hizi lakini niwombe tucheza kwa amani bila ya kufanya jambo lolote la kuashiria vurugu na tukitoka hapa tuache simulizi nzuri  mkoani hapa,”alisema Shelukindo.
Amesema wao kama wadhamini wa mchezo huo hawatapenda kuona nidhamu mbovu kwenye mchezo huo ambao sasa umekuwa ni mmoja wa michezo tishio nchini.

“Tucheze vizuri kwa kufuata sheria na kanuni za mchezo huu hadi mwisho ili uendelee kupendwa kama ulivyo sasa,”amesema.
Makamu mwenyekiti wa chama cha mchezo huo taifa (TAPA), Fredy Mush licha ya kuwapongeza wadhamini bia ya Safari Lager kwa kuutoa mbali lakini pia ameelezea kuridhishwa na viwango vya wachezaji wa timu zote 17 zilizoshiriki fainali hizo.
Mushi amesema kila mwaka viwango vya wachezaji vinaongezeka hali inayowapa imani ya kuwa mchezo huo sasa ni tishio nchini.
“Kwa kweli mchezo wa pool umefika pazuri maana kila mwaka tunashuhudia viwango vya wachezaji vikipanda hali inayoonyesha kuwa kuwa mchezo upo juu,”amesema Mushi.
Kabla ya fainali hizo kufunguliwa rasmi wachezaji  na viongozi wa chama cha mchezo huo taifa (TAPA) pamoja na meneja wa bia ya Safari Lager, Osacr Shaelukindo walitembelea wagonjwa katika hospitali  ya Rufaa ya Mawenzi ya mkoa wa Kilimanjaro na kutoa zawadi mbalimbali kwa wagonjwa.
Akizungumza baada ya wachezaji na viongozi wa TAPA kumaliza kutembelea wodi ya akinamama waliokwishajifungua na ambao hawajajifungua na wodi ya watoto,Kaimu Afisa Muuguzi Mkuu na Msimamizi  Wodi ya Wazazi, Fatima Rashid aliushukuru ugeni huo na kudai ni mfano wa kuigwa na vijana wengine.
“Kama mnavyojua wengine hapa hawana ndugu hivyo kuja kuwatembelea na kuwatelea zawadi kama hivi ni jambo zuri la kuigwa na wengine kwa kujenga tabia ya kutembelea kuwaona wagonjwa,”akasema Rashid

Timu zilizoshiriki fainali hizo na mikoa yao ikiwa kwenye mabano ni Blue Leaf (Lindi), Bilele (Kagera), Mpo Afrika (Temeke), Mashujaa (Ilala), Topland (Kinondoni), Yakwetu (Pwani), Billiard (Mwanza) na  New Stend (Shinyanga).
Nyingine ni  Delux (Dodoma),Black Point (Mbeya), Ngarenaro (Arusha), Nginja Master (Iringa), Corner Kasara (Manyara), Absom (Tanga),  Anatory (Morogoro), Tiptop (Tabora) na wenyeji  Mboya (Kilimanjaro).

No comments